Monday, March 26, 2012

Jamani Babu wa Kikombe, haya ni kweli?


Mchungaji msataafu wa Kanisa la Kiinjili la Kiluteri Tanzania, Ambilikile Masapile, anaendelea kusakamwa na wagonjwa wanaodai hawakuponeshwa na dawa yake, wapo walioweka nia ya kumburuza mahakamani lakini la kusikitisha zaidi ni kumfilisi. Wanaharakati wameeleza kuwa miongoni mwa mashtaka ambayo wanamfungulia Babu Ambi, mojawapo ni kumfilisi mali zote alizochuma endapo atakutwa na hatia ya ulaghai, wakati wa kutangaza maono aliyopewa na Mungu kuhusu tiba ya kikombe. Wanadai kuwa Babu Ambi, mkazi wa Kijiji cha Samunge, Loliondo, alitumia matatizo ya Watanzania ya kuugua maradhi sugu ili kujinufaisha, hivyo akatengeneza ulaghai wa tiba ya kikombe kwa maelezo kwamba ni ufunuo aliopewa na Mungu. Madai hayo yanakuja wakati ambao Babu Ambi ameukata, ameshakamilisha ujenzi wa nyumba yake ya kisasa kijijini Samunge, pia anamiliki magari mawili ya bei mbaya, Toyota Land Cruiser (pick-up) na Isuzu (pick-up). Babu Ambi, ameshahama nyumba chakavu aliyokuwa anaishi zamani na sasa anaendesha maisha yake kwenye nyumba mpya ya kisasa ambayo kwa Samunge, inaonekana ni kama Ikulu kwa jinsi inavyomeremeta.


Jamani wasomaji hiyo ndio ikulu wanaharakati na baadhi ya wagonjwa wa Babu wanailalamikia kuwa kawadanganya apate fedha za kujengea.



Wanaharakati wameenda mbali mpaka kubeza kuwa Babu hakustahili kuishi kwenye nyumba ndani vigae mpaka maliwatoni. Mpendwa msomaji hizi ni baadhi ya shutuma zinazomsibu Babu wa kikombe. Ulimwengu una mambo, wako wanaosema Babu kawarusha roho watu kwa manufaa yake binafsi na wako wanaodai kazifanyia kazi hela zilizotokana na uponyaji pia wako waliokaa kimya. Msomaji wewe uko upande gani? Watu walifumbwa macho muda wote ule tangu Babu alipoanza tiba mpaka alipojenga nyumba ndo wanastuka?
                                                                      


                                                                   

Monday, March 19, 2012

Askofu Salutaris Libena: Askofu wa kwanza Jimbo Katoliki Ifakara

                                                                              
Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, katika maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Yosefu, mchumba wake Bikira Maria, Msimamizi wa Kanisa, siku kuu inayofanyika kila mwaka tarehe 19 Machi, ameongoza Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumsimika rasmi Askofu Salutaris Libena kuwa askofu wa kwanza wa Jimbo Katoliki Ifakara ililoundwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, ili kusogeza huduma za kichungaji kwa waamini.


Askofu Libena aliwasili Jimboni Ifakara, Jumamosi tarehe 17 Mchi, 2012, na kupokelewa na umati mkubwa wa waamini na watu wenye mapenzi mema. Katika hotuba yake fupi, Askofu Telesphori Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro, alimtaka Askofu Libena kusimama kidete kulinda na kutetea imani na mafundisho ya Kanisa, bila kuogopa kwani wapo ndugu zake katika hurika wa uaskofu ambao wako tayari kumsaidia katika maisha na utume wake. Anawaalika Mapadre, watawa na waamini walei kutoa ushirikiano wa dhati kwa Askofu wao ili aweze kutekeleza majukumu yake ya: kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza watu wa Mungu Jimbo Katoliki Ifakara. Alipowasili, Askofu Libena na msafara wake wametembelea Parokia za Msolwa, Mkula na Kisawasawa. Jumapili tarehe 18 Machi, Askofu Libena ametembelea makao makuu ya Jimbo Katoliki Ifakara pamoja na Parokia ya Kibaoni. Jumapili jioni, katika Ibada ya Masifu ya Jioni, Siku kuu ya Mtakatifu Yosefu, aliikabidhiwa ufunguo wa Kanisa kuu.

                                                  
Askofu Agapiti Ndorobo wa Jimbo Katoliki Mahenge amewakumbusha waamini kwamba, kumegwa kwa Jimbo la Mahenge na kuundwa kwa Jimbo Katoliki la Ifakara kunapania kuboresha huduma za kichungaji kwa Familia ya Mungu Jimboni humo, changamoto kubwa iliyoko mbele yao ni Familia ya Mungu kuonesha ushirikiano wa dhati na Askofu Salutaris Melchior Libena.